Sunday, July 24, 2016

MOURINHO ACHEZEA KICHAPO CHA KWANZA KAMA KOCHA WA MAN UNITED

Jose Mourinho amepata kipigo kwa mara ya kwanza akiwa kama kocha wa Manchester United baada ya kushuhudia timu yake ikipata kipigo cha mabao 4-1 kutoka kwa Borussia Dortmund katika mchezo wa kombe la ‘International Champions Cup’ uliopigwa leo nchini China.
Dortmund ambao walikuwa wakicheza mchezo wa tano wa pre-season huku United wakicheza mchezo wao wa pili, walifanya kazi yao mapema na kufunga mabao mawili ya haraka na kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza.

Gonzalo Castro alifunga bao la ufunguzi kwa Borussia kabla ya Aubameyang kufunga lingine kwa penati baada ya beki wa Man United Antonio Valencia kunawa mpira ndani ya eneo la penati, baadaye kinda machachari wa timu hiyo Ousmane Dembele alifunga bao la tatu.
Henrikh Mkhitaryan, ambaye amejiunga na Man United hivi karibuni akitokea Borussia aliifungia bao pekee, kabla ya Castro tena kushindilia msumari wa mwisho baada ya kuachia shuti kali lililomshinda kipa wa Man United.
United ambao walikuwa wakicheza mchezo wa pili wa kwenye pre-season tour, walionekana kukosa umakini na uharaka langoni mwa wapinzani wao hasa kwa Mkhitaryan ambaye anaonekana kuhitaji michezo mingi zaidi kwa ajili ya kujiweka fiti, huku akiwasubiri Rooney na Ibrahimovic ambao wote bado wako mapumzikoni.
Kwa upande wa kocha wa Borussia Tuchel ameonekana kufurahishwa na kiwango cha timu yake huku akisubiri nyota wake wapya aliowaongeza ambao ni Mario Gotze na Andre Schurrle.

No comments:

Post a Comment